Pages

Subscribe:

Ads 468x60px

Thursday 13 January 2011

MWANZO WA MWISHO WA MICHANGO MIKUBWA YA SHEREHE

Naunga Mkono,wewe je?

From: Donath Olomi olomi@yahoo.com

Subject: MWANZO WA MWISHO WA MICHANGO MIKUBWA YA SHEREHE

Nimekuwa nafuatilia jinsi desturi ya kuchangia na kufanya sherehe kubwa inavyozidi kushika kasi, ikipelekea ule wigo wa kuomba michango kupanuka kiasi kwamba sasa hata mtu ambaye jina lako halijui vizuri anaweza kukuomba mchango.

Aidha michango na sherehe hizi zimekuwa mzigo mkubwa sana kwa baadhi ya watu, ikiwa ni pamoja na wale wenye kipato kidogo wanaochangiwa na kulazimika kulipa michango hiyo kwa miaka mingi. Je, wajua kuwa kuna familia ambazo zimefikia kulazimisha ndugu wauze mashamba au mifugo mtaji ili kupata fedha za kuchangia sherehe?. Je, wajua kuwa kuna watu ambao zaidi ya nusu ya kipato chao wanatumia kuchangia sherehe na huku wakishindwa kulipia huduma muhimu kama shule, matibabu, lishe, nk. Na kuwa wakati mwingine wewe au mimi (au wengine kama mimi na wewe) ndio wenyeviti na makatibu wa sherehe hiyo?. Na ni sisi tunaoona fahari ya kutumia milioni 30 au zaidi kwenye sherehe usiku mmoja?.

Kuna kijana mmoja jamaa yetu juzi juzi alipata shule Australia akawa anatafuta mchango wa dola 5,000 aende. Alipata 2,000 na amwekwama kwenda. Mwaka kesho akisema anaoa tutamchangia milioni 15-20!!!. Hii si hadithi, ni ukweli, na ni kielelezo cha ulimbukeni tuliofikia.

Siku za karibuni nimetambua kuwa kuna kundi kubwa tu linasikitishwa na huu mwenendo, na hata kutambua kuwa tunaweza kuwa tunaandikiwa dhambi kubwa (na hukumu yatusubiri) kwa jinsi wengi wetu tunashindwa kusaidia mambo ya msingi lakini tunakuwa wepesi kutoa kwenye sherehe. Wengi wanaamini kuwa tumeshatumbukia kwenye lindi la mazoea ambapo hatuwezi kujitoa mpaka upepo uje ubadilike wenyewe!.

Mimi nafikiri wasomi tuna jukumu muhimu la kuwa chachu ya mabadiliko pale ambapo mazoea yenye madhara yanavuka mipaka na kuweza hata kuwa chanzo cha ufukara na kuviza maendeleo.

Ili kubadilisha hili jambo, lazima tuanzie mahali. Mimi napendeleza na kuanza kutekeleza. Kuanzia Januari 2011, nitapunguza michango ninayotoa. Nitatoa tu kwa mtu wa karibu sana , na nitachanga kidogo. Usishangae nikakuchangia 20,000/= kama ulitegemea 50,000/= kwa mfano. Kuanzia July 2011, nitaacha kabisa kuchangia sherehe. Badala yake nitakuwa nachangia elimu pale ambapo mzazi hayupo au mhusika kweli hana uwezo na pia nitachangia miradi mingine ya jamii na maendeleo.

Je waniunga mkono? Kama ndiyo sambaza huu ujumbe kwa mtandao wako.

Dr. D.R.Olomi

Box 35036 Dar es Salaam , Tanzania

5 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Hakika huu ni ulimbikeni haswa na naungana mkona na Dr.DR Olomi. Na Edna asante kwa kuuweka hapa ujumbe huu.

emu-three said...

Sijui utawaambianini wapenda harusi, tumejaribu kulipinga hili lakini mmmh, jamani watu wanapenda hizi shughuli, we acha tu...kesho na kesho kutwa mtu huyu huyu aliyechanga hela kibao kwenye shughuli anatafuuta ada za watoto

EDNA said...

Yasinta: kweli ni ulimbukeni uliopitiliza,watu tunayapa kipaumbele mambo ambayo hayana hata msingi.

Emu 3- Tena usipowachangia wanakutenga kwa kudai kuwa huna ushirikiano na wanajamii wenzako mweee.

Joyce said...

Mawazo yako ni mazuri sana tena ni ya maendeleo, big up baba!!!.....umeongelea sherehe za harusi tuu...je misiba inakuwaje????

Joyce said...

Mawazo yako ni mazuri sana tena ni ya maendeleo, big up baba!!!.....umeongelea sherehe za harusi tuu...je misiba unafanyaje inapokuwa amefariki mtu wa karibu????