skip to main  |
      skip to sidebar
          
        
          
        
INAKUHUSU WEWE ULIYE NDANI YA NDOA.
 

 
Inahuzunisha lakini kuna fundisho kuu kwetu sote.
 “Nilipofika nyumbani usiku ule, mke wangu aliponitayarishia chakula, 
nilimshika mkono na kumwambia, Kuna kitu nataka nikwambie. Mke wangu 
alikaa chini na kula chakula kimya akiwa tayari kunisikiliza. Tena 
nikagundua macho yake yalionyesha anaumizwa. Nilishindwa hata namna ya 
kuanza kufumbua kinywa changu. Lakini ilibidi nimwambie ili ajue 
nilikuwa nikifikiri nini juu yake.
 
 Nataka kukupa talaka. 
Nilianza kusema kwa utulivu. Alionekana kutokereka na maneno yangu 
badala yake aliniuliza kwa sauti ya upole ‘kwa nini?’ Sikumjibu swali 
lake. Kutojibu kulimfanya akasirike. Akatupa kijiko na akanikaripia, 
‘wewe si mwanamume!’ Usiku ule, hakukuwa na maongezi kati yetu. Alikuwa 
akilia kwa kwikwi. Nilifahamu kwamba alitaka kujua ni nini kimetokea 
kwenye ndoa yetu. Lakini kwa hakika nisingeweza kumpa jibu wala sababu 
ya kuridhisha; alionekana si mali kitu kwangu penzi langu lilihamia kwa 
Jane. Sikumpenda tena mke wangu mawazo yote yalikuwa kwa Jane. Kwa kweli
 nilimdharau mke wangu!
 
 Huku moyo wangu ukijua wazi kwamba 
nafanya kosa, niliandika talaka ambayo ilionyesha kwamba yeye (mke 
wangu) angepata nyumba yetu, gari na atakuwa na hisa 30% ya kampuni 
yetu. Aliangalia talaka ile na kuichana vipande vipande.
 
 Mke 
ambaye tumeishi nami kwa miaka 10 alionekana mgeni machoni mwangu. 
Nilimuonea huruma kwa muda, rasilimali na nguvu alizopoteza lakini 
sikuweza kurudi nyuma kwa sababu Jane aliuteka moyo wangu kisawasawa. 
Hatimaye mke wangu alilia kwa sauti mbele yangu, jambo ambalo kwa hakika
 nilitarajia. Kwangu mimi kilio chake kilinipa nafuu.
 
 Wazo la kuachana na mke wangu limenisumbua kwa majuma kadhaa na sasa limeendelea kuimarika na kuwa jambo la hakika zaidi.
 
 Siku iliyofuata nilikuja nyumbani kwa kuchelewa sana nikakuta mke wangu
 akiandika jambo mezani. Sikutamani hata kula chakula alichonipikia 
nilikwenda moja kwa moja chumbani na usingizi ulinichukua mara moja kwa 
sababu nilikuwa nimechoka baada ya kula raha za kufa mtu na Jane.
 
 Usiku nilishtuka usingizini mke wangu alikuwa bado akiandika. Sikujali 
kabisa nikajifunika vyema shuka na kulala tena. Asubuhi yake 
alinikabidhi masharti ya talaka yake: hakutaka kitu chochote kutoka 
kwangu lakini alihitaji apate angalau mwezi mmoja wa kujiandaa kabla 
hajaachika. Akaomba kwamba katika kipindi hicho cha mwezi mmoja sote 
mimi na yeye tujitahidi kuishi maisha ya upendo au kawaida kwa kadiri 
itakavyowezekana. Sababu yake ilikuwa ndogo lakini muhimu: mwanetu wa 
kiume alikuwa akikaribia kufanya mtihani katika mwezi uliofuata kwa hiyo
 hakupenda mtoto aathirike kisaikolojia kwa sababu ya kuachana kwetu. 
Hili halikuwa tatizo kwangu, nilikubali mpango wake. Lakini alikuwa na 
sharti la ziada, aliniomba nikumbuke jinsi nilivyombeba siku za fungate 
yetu hasa siku ya harusi yetu. Akaniomba na kunisihi kwamba katika 
kipindi hicho cha mwezi mmoja niwe nambeba kutoka kitandani kwetu mpaka 
mlango wa kutokea kila asubuhi. Nilidhani anakaribia kuwa kichaa. Ili 
kufanya siku zetu za mwisho zisiwe na migogoro nilikubaliana na masharti
 yake ya ajabu.
 
 Nilimsimulia Jane kuhusu masharti ya kuachana 
na mke wangu. Jane alicheka sana, aliona ni ujinga. ‘Hata akitumia 
ujanja wa namna gani talaka ni lazima’, alisema Jane tena kwa dharau. 
Mimi na mke wangu hatukuwahi kugusana tangu nilipomweleza dhamira ya 
kumtaliki. Kwa hiyo nilipombeba kwa mara ya kwanza sote tulinuniana. 
Mwanetu alifurahi sana na kupiga makofi nyuma yetu, ‘aah baba kambeba 
mama mikononi mwake’. Maneno yake yalinichoma moyoni moja kwa moja. 
Kutoka chumbani kwetu hadi sebuleni, halafu tena mpaka mlangoni, ni 
zaidi ya mita kumi nimembeba mke wangu. Alifumba macho na kusema kwa 
sauti laini na ya upole; usimwambie mwanetu juu ya talaka. Nilikubali 
kwa kichwa, ingawa nilijisikia vibaya. Nilimuweka chini nje ya nyumba.
 
 Alienda kituoni kusubiri basi la kazini kwake nami nikaendesha gari 
kwenda ofisini kwangu. Siku ya pili, zoezi lilikuwa rahisi kwetu sote. 
Aliegemea kifuani pangu. Nilisikia harufu nzuri ya uturi aliofukiza 
kwenye blauzi yake. Nikagundua kwamba sijamuangalia kwa makini mke wangu
 kwa kipindi kirefu sana. Nikagundua hakuwa binti tena. Kulikuwa na 
mikunjo usoni na nywele zake zilianza kuwa nyeupe! Ndoa yetu imekula 
urembo wake. Kwa dakika moja nikafikiri kwa nini namfanyia hivi.
 
 Siku ya nne nilipombeba hisia za mapenzi kati yetu zilirejea. Huyu ni 
mwanamke aliyejitoa kuishi nami na tumeishi kwa miaka kumi sasa. Siku ya
 tano na ya sita ilikuwa wazi kwamba mapenzi yetu yalikuwa yakimea upya.
 Sikumwambia Jane kuhusu jambo hili. Kadiri mwezi ulivyokaribia kwisha 
niliona raha kumbeba mke wangu na zoezi likawa rahisi zaidi. Pengine 
kufanya kazi hii kila siku kuliniimarisha zaidi.
 
 Alikuwa 
akichagua nini cha kuvaa asubuhi. Alichagua mavazi kadhaa hakupata 
linalomfaa. Kisha akaguna, ‘nguo zangu zote zimekuwa kubwa’. Nikagundua 
kwamba mke wangu amepungua sana, nadhani ndiyo maana niliweza kumbeba 
kirahisi. Ghafla jambo likanichoma... mke wangu ana uchungu na maumivu 
makuu moyoni mwake. Bila kujitambua nikamgusa kichwa chake. Mara mtoto 
wetu akatokeza na kusema ‘baba ni wakati wa kumbeba mama muende kazini’.
 Kwake kumuona baba akimbeba mama likawa ni jambo la furaha sana. Mke 
wangu alimuonyesha ishara mwanetu asogee karibu na akamkumbatia kwa 
upendo mkuu. Niligeuza uso wangu nisije nikabadili mawazo katika dakika 
ya mwisho. Kisha nikambeba mikononi mwangu kutoka chumbani, sebuleni 
halafu mpaka mlangoni. Mkono wake laini ulikuwa umeizunguka shingo yangu
 kwa upendo. Nilimkumbatia mwili wake; ilikuwa ni mithili ya siku ya 
ndoa yetu. Lakini wepesi wake ulinitia mashaka.
 
 Siku ya mwisho 
nilipombeba nilipata shida hata kupiga hatua moja. Mtoto wetu 
alishakwenda shuleni. Nilimshika kwa karibu na kumwambia sikubaini 
kwamba maisha yetu yalikosa upendo. Nikaenda zangu ofisini…. Nikashuka 
garini hata bila kufunga mlango. Maana nilihisi nikichelewa tu ninaweza 
kubadili nilichoamua.... nikapand ngazi. Jane alifungua mlango 
nikamwambia, ‘Samahani, Jane, sihitaji tena kumtaliki mke wangu’. 
Akaniangalia kwa kustaajabu, halafu akagusa kichwa changu. Akaniuliza 
‘Unaumwa?’ Nikaondoa mkono wake kichwani kwangu. ‘Samahani, Jane, 
nimesema sitaki kumtaliki mke wangu. Nadhani ndoa yangu haikuwa na 
furaha kwa sababu sikuthamini undani wa maisha yetu, mimi na mke wangu, 
si kwamba hatupendani. Nimetambua hilo tangu nilipombeba siku ya ndoa 
yetu nilitakiwa kumbeba siku zote za maisha yetu, nampenda mke wangu 
sitamuacha mpaka kifo kitakapotutenganisha.’
 
 Ikawa kama Jane 
alizinduka usingizini. Akanizaba kibao cha nguvu, akajiegemeza mlangoni 
na kuanza kulia. Nikashuka ngazi na kuondoka zangu. Nikaingia kwenye 
duka la maua nikaagiza maua mengi mazuri kwa ajili ya mke wangu. Muuzaji
 akaniuliza aandike nini kwenye kadi. Nikatabasamu na kuandika 
“Nitakubeba kila asubuhi mke wangu mpaka kifo kitakapotutenganisha”. 
Jioni ile nilifika nyumbani na maua mikononi mwangu, tabasamu kubwa 
usoni nikakimbia mpaka chumbani, nikapokelewa na maiti ya mke wangu 
kitandani.
 Kumbe mke wangu alikuwa akisumbuliwa na saratani kwa 
miezi kadhaa nami nilishindwa kubaini kwa sababu nilihamishia akili 
yangu kwa Jane. Alijua kwamba angekufa karibuni na alitaka asiniingize 
katika chuki na mwanetu kama ningelazimisha talaka mapema.
 Angalau machoni mwa mwanangu naonekana ni mume mwema….
 
 Jamani vitu vidogo vidogo vizuri ni vya msingi sana katika mahusiano 
yetu... Siyo majumba au magari au fedha zilizoko kwenye benki. Hivi 
vitakupa tu mazingira ya kufurahi lakini vyenyewe siyo furaha. Kwa hiyo 
jitahidi kuwa na muda mzuri na mazingira rafiki ya kuwa na mwenzi wako, 
kuwa rafiki wa mwenzi wako. Fanya vitu mlivyofanya wakati wa uchumba na 
wa ndoa yenue ambavyo vitawaweka karibu siku zote. Muwe na ndoa yenye 
furaha. Mara nyingi watu hushindwa katika ndoa kwa kutotambua ni kwa 
kiasi gani walikuwa karibu wakati wa kujenga uhusiano wao
 Mungu awabariki nyote mliosoma na kujifunza hapa.
CREDIT TO FACEBOOK MKE/MUME MWEMA GROUP. 
 
 
 
          
      
 
 
 
 
 
 
  
  
4 comments:
Hakika ni fundisho kubwa sana kwa wenye ndoa..nampongeza sana mwanamke huyu..
Mmmhh Asante kwa somo mwanakwetu..Pamoja sana.
Ameeen..!!
Swali: Hivi kuna mafundisho kwa wanaume kabla ya ndoa?..kama kwa wanawake kitchen party..
@Mija Shija,sina uhakika kama hayo mafundisho yapo,Ila ninachojua kwa wakristo huwa kuna kuwa na semina kanisani kwa wanaume na wanawake kabla ya ndoa.
Post a Comment